Monday, October 8, 2012

CRISTIANO RONALDO AWEKA REKODI MPYA 'EL CLASICO' KATI YA REAL MADRID NA BARCELONA



MADRID, Hispania 

Cristiano Ronaldo ametokea kuwa na 'mzuka' wa kupachika mabao kila mara anapocheza dhidi ya Barcelona na amethibitisha hilo kwa mara nyingine jana usiku pale alipofunga mabao yote mawili ya Real Madrid wakati wakitoka sare ya 2-2 dhidi ya Barca katika 'el clasico' yao ya La Liga, Ligi Kuu ya Hispania.

Kutokana na mabao aliyofunga jana  kwenye Uwanja wa Camp Nou, Ronaldo ameandika rekodi kwa kuwa mchezaji wa kwanza katika historia kuwahi kufunga katika mechi sita mfululizo za 'el clasico' ya mahasimu wa jadi, Barcelona na Real Madrid.

Ronaldo alianza kasi yake katika robo fainali ya Kombe la Mfalme msimu uliopita, akifunga katika mechi ya kwanza kwenye Uwanja wa Santiago Bernabeu na ya marudiano kwenye Uwanja wa Camp Nou.

Aliendeleza makali yake katika mechi ya marudiano ya La Liga, Ligi Kuu ya Hispania iliyochezwa April 21 wakati alipofunga goli lililowapa Real Madrid ushindi wa 2-1 na kuwasafishia njia ya kutwaa ubingwa msimu uliopita wa 2011/2012.

Wakati walipokutana katika mechi mbili za kuwania taji la Super Cup mwanzoni mwa msimu huu, Cristiano pia alifunga katika mechi zote na kuisaidia Real kutwaa taji hilo kabla ya jana kufunga tena mabao yote mawili ya Real Madrid.

No comments:

Post a Comment